Mbwana Samatta anavalia jezi namba 77 halafu amefunga goli la kusawazisha dakika ya 77 zikiwa zimesalia dakika 13 mchezo kumalizika
Mbwana Samatta ameifungia bao la kusawazisha Genk katika sare ya 2-2 na Liege Uwanja wa Laminus Arena mjini Genk.
Mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Tanzania katika mechi ya Jumapili ameinusuru timu yake, KRC Genk kulala nyumbani mbele ya Standard Liege katika mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza A Ubelgiji.
Mchezaji huyo wa zamani wa Simba alifunga bao hilo dakika ya 77 akimalizia pasi ya beki Jere Uronen kutoka Finland.
Katika mchezo huo, ambao mshambuliaji wa Uganda, Faruk Miya alikuwa kwenye benchi la Liege muda wote, Genk walikuwa wa kwanza kupata bao lililofungwa na beki Mgambia Omar Colley dakika ya tatu, akimalizia pasi ya mshambuliaji Mjamaica, Leon Bailey.
Standard Liege ikatoka nyuma na kuongoza kwa 2-1 kwa mabao ya washambuliaji Mreno Orlando Sa dakika ya 15 na Mualgeria Ishak Belfodil dakika ya 25.
Huo unakuwa mchezo wa 35 jumla kwa Samatta kucheza Genk tangu awasili Januari mwaka huu kutoka TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC),18 msimu uliopita na 17 msimu huu.
Kati ya hizo, ni mechi 17 tu alianza, 10 msimu uliopita na saba msimu huu, 18 alitokea benchi, nane msimu uliopita na 10 msimu huu, wakati nane hakumaliza baada ya kutolewa, sita msimu uliopita na mbili msimu huu huku akiwa amefunga jumla ya mabao tisa, manne msimu huu na matano msimu uliopita.